Ajali ya Lori na Pawatila Yaua Watu 7 Manyara


Watu saba wamekufa na wengine saba kujeruhiwa katika ajali ya gari iliyotokea katika kijiji cha Endagau tarafa ya Endasaki wilayani Hanang’ mkoani Manyara baada ya lori aina ya Fuso kugongana na powatila.
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Christopher Fuime alisema lori hilo yenye namba za usajili T 781 AAC likitokea Katesh kuelekea Babati liligongana na pawatila iliyokuwa imebeba wakulima waliokuwa wakitokea shambani kuvuna maharage katika kijiji cha Getasam.
 
Kamanda Fuime alisema kwamba chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa fuso ambapo lilisababisha kupasuka kwa gurudumu la mbele ndipo lilipoteza mwelekeo na kuligonga pawatila na kusababisha watu sita kufa papo hapo na mmoja kupoteza maisha katika Hospitali ya Dareda wakati akipatiwa matibabu.
 
Aliwataja waliokufa ni Uttu (18) Mkazi wa Endasaki, Lazaro Daniel (30) mkazi wa Kijiji cha Maraa, Agustino Marcel (30) mkazi wa Kijiji cha Maraa, Inocent (16) Mkazi wa Maraa, Stephano Dahaye (18) Mkazi wa Maraa, Michael Faustine (25)Mkazi wa Maraa na Elias Leonce (18) naye mkazi wa Mara aliyefariki dunia akiwa hospitalini.
 
Aidha Kamanda Fuime aliwataja waliojeruhiwa katika ajali hiyo kuwa ni Godfrey Samwel (17), Daniel Yamee (17), Amani Rajabu (19), Isaya Joseph (25), Hemed Darabe (25), Inocent Ploti na Paulo Anjelus (16) wote wakazi wa Mara.
 
Hata hivyo, Kamanda Fuime alisema kuwa jeshi la polisi linaendelea na juhudi za kumtafuta dereva wa Fuso aliyekimbia baada ya kusababisha ajali hiyo.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini