Rais Kikwete Apokea Ripoti Ya Oparesheni Tokomeza



Rais Jakaya Kikwete jana alipokea Ripoti ya Uchunguzi wa Operesheni Tokomeza katika hafla fupi ilifanyika Ikulu, Dar es Salaam.
 
Mara baada ya kupokea ripoti hiyo, Rais Kikwete aliishukuru Tume kwa kazi nzuri na kuongeza kuwa amefurahi kuwa suala zima la Operesheni Tokomeza sasa limefika mwisho wake.
 
Aidha, Rais amesema kuwa Serikali itaisoma ripoti hiyo na katika wiki mbili itatoa maelezo ya jinsi ripoti hiyo itakavyoshughulikiwa.
 
Rais Kikwete amepokea ripoti hiyo kutoka kwa Jaji mstaafu Hamisi Msumi, Mwenyekiti wa Tume ambayo Rais Kikwete aliiteua Mei Mosi, mwaka jana, na kuitaka ichunguze tuhuma mbali mbali za uvunjifu wa Sheria, Kanuni, Taratibu na Hadidu za Rejea za Utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.
  
Aidha, Rais Kikwete aliipa Tume hiyo jukumu la kupendekeza hatua stahiki za kisheria za kuchukua dhidi ya watakaobainika kuhusika na uvunjifu huo. Vile vile, Rais aliiagiza Tume hiyo ishauri namna bora ya utekelezaji wa operesheni kama hiyo hapo baadaye.
 
Rais Kikwete pia aliipa Tume hiyo hadidu za rejea sita ambazo pia ziliainishwa katika Taarifa ya Serikali Nambari 131 ya 2014.
 
Hadidu za Rejea hizo ni kama zifuatazo: Kuchunguza namna Operesheni Tokomeza ilivyotekelezwa, kuchunguza iwapo maofisa waliotekeleza Operesheni Tomokeza walizingatia sheria, kanuni, taratibu na hadidu za rejea walizopewa, kuchunguza iwapo maofisa waliotekeleza Operesheni Tokomeza walivunja sheria, kanuni, taratibu na hadidu rejea walizopewa.
 
Nyingine ni kuchunguza iwapo kuna watu waliokiuka sheria yoyote wakati wa utekelezaji wa Operesheni Tokomeza na iwapo hatua zilizochukuliwa na maofisa wa Operesheni Tokomeza dhidi ya wakosaji hao na mali zao zilikuwa sahihi.
 
Pia walitakiwa kupendekeza hatua zinazostahili kuchukuliwa dhidi ya maafisa wa Operesheni Tokomeza waliokiuka sheria, kanuni, taratibu na hadidu za rejea za Operesheni Tokomeza; na Nyingine ni kupendekeza mambo yanayopaswa kuzingatiwa wakati wa kupanga na kutekeleza Operesheni nyingine kama hii, ili kuepuka malalamiko mengine yasitokee.
 
Jaji Msumi amemweleza Rais Kikwete kuwa katika kutelekeza majukumu yake, Tume ilitembelea mikoa 20 na wilaya 38 na kupokea malalamiko mbali mbali kutoka kwa viongozi wa Serikali ikiwa ni pamoja na mawaziri wanne waliojiuzulu kutokana na sakata hilo.
  
Pia ilipokea malalamiko kutoka kwa watekelezaji wa Operesheni; na walalamikaji na waathirika wa Operesheni.
 
Jaji Msumi amemweleza Rais Kikwete kuwa Ripoti ya Tume ina juzuu kumi, juzuu ya kwanza ikiwa ni Muhtasari wa Taarifa ya Tume, juzuu ya pili ikiwa ni Taarifa yenyewe ya Tume, Juzuu ya tatu hadi ya tisa ikiwa ni Mwenendo wa Ushahidi (Proceedings) na Juzuu ya kumi, ikiwa ni vielelezo vilivyotolewa na mashahidi.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini