ATESEKA KITANDANI MIAKA MITATU NI BAADA YA KUPEWA TAARIFA YA KIFO CHA BABA YAKE



INASIKITISHA! Johanitha Robert Mulokozi (31) amekuwa kitandani kwa miaka mitatu kutokana na kuugua ugonjwa wa kupooza mwili mzima.Mama huyo mwenye mtoto mmoja amekuwa akisumbuka na ugonjwa huo uliomfanya akose raha licha ya kupata matibabu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
 
Johanitha Robert Mulokozi amekaa kitandani kwa miaka mitatu kutokana na kuugua ugonjwa wa kupooza mwili mzima.
Akizungumza na waandishi wetu nyumbani kwake Nyan’gandu, Kivule, Ilala jijini Dar es Salaam, mama wa mgonjwa huyo, Valentina Emmanuel (51) alisema kwa miaka mitatu anashindwa kupata usingizi kutokana na kumuuguza mwanaye huyo na kukosa uwezo wa kumsafirisha kwenda India kwa matibabu.
Akisimulia huku akilengwalengwa machozi Valentina alisema: “ Tatizo la mwanangu la kupooza mwili mzima lilianzia pale alipodondoka chini baada ya kupata taarifa za kifo cha baba yake mwaka 2011.
“Sikutegemea kama mwanangu angekuwa hivi kwani alikuwa akiishi vizuri na alikuwa akiendelea na maisha yake hasa baada ya kupata mtoto ambaye anamtegemea.
“Baada ya kupata tatizo hili nilimpeleka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na alilazwa pale kwa matibabu lakini hali bado ikawa mbaya.
“Ninachoweza kusema mimi ni kwamba sikukata tamaa, niliendelea kufanya juhudi kuokoa maisha yake licha ya kulazwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa muda wa miezi sita pasipo kupata nafuu na kuamua kumrudisha nyumbani.
 
Johanitha Robert Mulokozi akiwa nyumbani kwao Kivule, Ilala jijini Dar es Salaam.
“Baadaye nilipata wazo la kumpeleka katika Hospitali ya Regence jijini Dar na nilipofika pale na kuwaelezea tatizo la mwanangu, walimpima na madaktari walibaini kuwa tatizo lake linaweza kutibika nchini India, nikaambiwa nitafute shilingi milioni kumi na tatu. Nilishika kichwa na kuanza kulia.
“Nililia kwa sababu nilijiuliza, nitapata wapi fedha hizo niokoe maisha ya mwanangu. Niliamua kumfuata Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa na kumuelezea tatizo langu.
“Namshukuru sana baba yule (Jerry) kwani baada ya kumpa maelezo na kumuonesha barua ya safari ya India aliingiwa na huruma , akaniandikia hundi ya shilingi milioni sita (6,000,000/), hivyo nina upungufu wa shilingi milioni saba ili mwanangu aweze kupelekwa India kwa matibabu,” alisema mama huyo huku akifuta machozi kwa kanga yake.
Mgonjwa hakuweza kuzungumza na gazeti hili na badala yake wakati wote wa mahojiano na mama yake alikuwa akilia wakati wote.
Yeyote aliyeguswa na tatizo la mama huyu na angependa kumsaidia mchango anaweza kuwasiliana naye kwa namba ya simu, 0714599104, 0754086888.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini