DUNIA INA MAMBO: MUME AUA MTOTO, AJIUA KISA MESEJI

Busia, Kenya. Mkazi wa Mji wa Kisoko, Philip Wandera (27) amejitupa na wanawe wawili katika Mto Sio, baada ya kuzozana na mkewe kuhusu ujumbe mfupi(sms) alioupata katika simu yake.

Wandera, aliyejitupa mtoni na simu ya mkewe, alifariki dunia na mwanaye mmoja. 

Mmoja wa mashuhuda, Mary Onyango, alidai kuwa Wandera alikuta ujumbe katika simu ya mkewe uliokuwa umetumwa na mwanaume mwingine. 

“Walianza kupigana na mkewe alikimbilia nyumbani kwa shangazi yake. Lakini kutokana na hasira aliyokuwa nayo, mwanaume huyo aliwachukua wanawe wawili wakiwa wamelala na kuwarusha ndani ya maji na yeye mwenyewe kujizamisha. Mmoja wa wanawe wa kiume alinusurika,” alisema Onyango. 

Mtoto huyo aliyenusurika alisimulia wenyeji kuwa baba yake alikuwa amemwambia akae ukingoni mwa mto na kumtazama akifa, kisha wawafahamishe jamaa zake.

“Ingawa kulikuwa na giza, nilimuona babangu akizama, kabla ya kumweleza nyanyangu (bibi) kilichotokea,” alieleza. 

Mama wa marehemu, Sebencis Odembo alisema mwanawe alikuwa amerejea nyumbani kutoka Nairobi Jumatatu iliyopita kumjengea mkewe nyumba kabla ya tukio hilo kutokea.

Odembo alisema mwanawe alirudiana na mkewe hivi karibuni baada ya kutengana kwa muda mrefu. 

Chifu wa eneo hilo, Peter Khayo alilalamikia ongezeko la watu kujiua na kuwataka watu kutafuta usaidizi kutoka Serikalini badala ya kujiua na kuua watoto wasiokuwa na hatia.

Ofisa mkuu wa polisi wa Nambale, Moss Ndiwa alisema wameanzisha uchunguzi wa tukio hilo.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini