KESI YA DAWA ZA KULEVYA ZA MABILIONI ZAWAFIKISHA MAHAKAMANI WATU HAWA HAPA

WATU watano akiwemo raia wa Uingereza wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, wakikabiliwa na mashitaka ya kukutwa wakisafirisha gramu 2870.781.36 za dawa za kulevya zenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni tano.

Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo jana na kusomewa mashitaka manne mbele ya Mahakimu wawili tofauti. Washitakiwa hao ni raia wa Uingereza Halid Mahunga, wafanyabiashara Anna Mboya, Fred William, Kambi Zuberi na Hamis Mtou (32), wakazi wa Dar es Salaam.
 
Katika mashitaka yanayomkabili Mboya, Wakili wa Serikali Mwandamizi Evetha Mushi alidai mbele ya Hakimu Mkazi Hellen Riwa kuwa Januari 2, mwaka 2011 Mboya akiwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere alikutwa akiingiza nchini gramu 1195.45 dawa za kulevya aina ya cocaine zenye thamani ya Sh 46,296,200.
Washitakiwa wengine William na Zuberi walifikishwa mbele ya Hakimu Riwa na kusomewa mashitaka ya kuingiza nchini dawa hizo zenye thamani ya Sh 5,262,341,700.
Wakili wa Serikali alidai kuwa washitakiwa wanadaiwa Februari 21, 2011 walikutwa Mbezi Jogoo, Wilaya ya Kinondoni wakisafirisha gramu 175.411.36 ya dawa za kulevya aina ya heroine zenye thamani hiyo.
Katika mashitaka yanayomkabili Mtou, Wakili wa Serikali Mwandamizi Rose Chilongozi alidai mbele ya Hakimu Mkazi Warialwande Lema kuwa Novemba 17, 2010 mshitakiwa akiwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere alikutwa akisafirisha gramu 811.54 ya dawa za kulevya aina ya heroine zenye thamani ya Sh 24,346,200.
Aidha katika kesi inayomkabili Mahunga, Mwendesha Mashitaka Thadeo Mwenemtazi alidai mbele ya Hakimu Lema kuwa Februari 16, 2010 mshitakiwa alikutwa akisafirisha kete 69 aina ya cocaine gramu 107.40 zenye thamani ya Sh 50,370,000 kutoka Tanzania kwenda Uingereza.
Katika shitaka la pili Mahunga anadaiwa siku hiyo hiyo alikutwa akisafirisha gramu 581.38 za dawa hizo aina ya bangi zenye thamani ya Sh 58,138.
Baada ya washitakiwa kusomewa mashitaka yao hawakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa Mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hizo isipokuwa Mahakama Kuu.
Wamerudishwa rumande, kesi zote upelelezi ukiwa umekamilika na watasomewa maelezo ya kesi yao Machi 2 na Machi 3, mwaka huu.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini