Mtoto wa Johari Anaeyesemekana Aliyejifungua Kwa Siri Azua Maswali Mengi


Johari
BRIGHTON MASALU
KUFUATIA kuibuka kwa habari ya msanii nguli, Blandina Chagula ‘Johari’ kubeba mimba na kujifungua kwa siri hadi mtoto kufikisha umri wa miezi 7 na kuripotiwa kwa mara ya kwanza na gazeti ‘tumbo moja’ la hili la Risasi Jumamosi, mambo mengi mapya ikiwemo maswali yameibuka na kuzua ‘sintofahamu’ juu ya uhalisia wa jambo hilo, Amani linakupa mchapo kamili.

Saa chache baada ya habari hiyo kusomwa na mamilioni ya Watanzania wakiwemo wadau wa sanaa na burudani wiki iliyopita, minong’ono na mishangao ilianza kutambaa ambapo wengi walidadisi kwa kina ili kujua ‘lipi ni tui la nazi na yapi ni maziwa’ juu ya habari hiyo.

MASWALI YALIYOIBULIWA
Miongoni mwa maswali yaliyoibuliwa ni pamoja na mimba aliibeba akiwa wapi? Alitoka Dar kwenda Shinyanga anakodai kujifungulia mimba ikiwa na muda gani? Anaweza kuianika kadi ya kliniki? Nini sababu ya kuficha mimba hadi mtoto anafikisha miezi 7 na nini kimemsukuma kumwanika mtoto?

“Jamani, mbona hatuelewi haya mambo? Hivi inawezekana kweli kwa mtu maarufu kama Johari kubeba mimba na hadi kujifungua na mtoto kufikisha miezi yote hiyo (7) bila kujulikana?” alihoji Latifa Lusengi wa Sinza- Makaburini.
“Hiyo mimba aliibebea wapi? Mbona alikuwa akionekana hana tumbo?” alihoji mama Jane wa Mwananyamala.

MASTAA SASA
Kuashiria kuwa mjadala ulikuwa mzito, hoja na maswali hayakuishia kwa wadau tu kwani hata baadhi ya mastaa waliozungumza na mwandishi wetu ama ana kwa ana au kwa njia ya simu kwa nyakati tofauti, walionesha wasiwasi mkubwa juu ya habari ya utata huo huku wengine wakiomba hifadhi za nomino zao kwa kile walichokiita ni “kujitunzia heshima kwa Johari.”


MAINDA
Ruth Suka ‘Mainda’ ndiye alifungua pazia la majadala huu kwa upande wa mastaa, baada ya mwandishi wetu kumpigia simu na kumtaka atoe maoni yake juu ya kujifungua kwa ‘mbia’ wake huyo.“Mmh! Kama kweli Johari amejifungua, basi mimi nampongeza kwani kuzaa ni baraka, lakini sasa afikirie na suala la kufunga ndoa na huyo aliyezaa naye kwani hata umri unamruhusu, asikomee tu mtoto.”

“Nyie acheni utani bwana, sisi tunashinda naye kila siku iwe baa au sehemu tofauti, mbona hatukuona hata hizo dalili na ishara za mimba na sisi wanawake tunajuana sana kwa mambo kama hayo? Sijui lakini,” alihoji  msanii mwingine wa kike ambaye amekuwa akionekana mara kwa mara na Johari na kuomba hifadhi ya jina.
“Kama ni kweli kulikoni afiche mimba?” aliuliza kwa kifupi msanii wa kiume.

JOHARI AZIDI KUPIGILIA MSUMARI
Baada ya mwanahabari wetu kusikia maswali hayo kutoka kwa wadau na baadhi ya wasanii, alimtafuta Johari kupitia simu yake ya kiganjani ambapo alifunguka, kisha kukata simu.

“Mimba niliibebea tumboni, kwani kwa mwanamke kuzaa ni tatizo? Au walitaka niutangazie ulimwengu kuwa nimebeba mimba na nitajifungua siku fulani? Siko hivyo bwana.“Wanaotangaza hadi siku za kubeba mimba ni wao na umaarufu wao, mimi ni mtu mzima, naomba nilale kwanza, nina usingizi sana nitakutafuta baadaye,” alisema Johari na kukata simu na kuizima kabisa.

KUTOKA AMANI
Kuzaa ni jambo la heri, tunamuomba Johari kukata kiu ya maswali yote ya wadau na mashabiki wake ili kuondoa mkanganyiko, ikiwezekana aanike cheti cha mtoto ili kuwakata ‘vilimi’ wale ambao hawataki kuamini kile anachokizungumza. Hakuna sababu ya kufanya jambo lenye baraka na neema kama hili kuwa siri na kuficha wakati yeye ni mtu maarufu–Mhariri.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini