Suala la usajili Yanga sasa lawa 'serious' Mwaka Huu...Hichi Ndicho Walichoamua Hakuna Mzaha Tena

KLABU ya Yanga imesema kutokana na mkakati wao wa kusuka kikosi cha kufa mtu cha msimu ujao, hawatakuwa na mzaha katika usajili wao kwa kusubiri kuletewa wachezaji na wanaojiita mawakala.

Badala yake, Wanajangwani hao wameamua kujitosa ‘jumla jumla’ kufuatilia wachezaji waliong’ara katika timu zao msimu uliomalizika hivi karibuni na kuona kama wanaweza kuwasajili.
Katibu Mkuu wa Yanga, Jonas Tiboroha, alisema jana kuwa wamebaini wachezaji wengi wanaoletwa na wanajiita mawakala kufanya majaribio hapa nchini, si lolote zaidi ya kuja kuganga njaa.
Alisema kwa kutambua hilo, wamejipanga kuhakikisha wanasafiri katika eneo lolote la Bara la Afrika kumfuata mchezaji ambaye atabainika kuwa na kiwango cha juu.

“Hatutasubiri kuletewa mchezaji na wakala, wengi wanaokuja kufanya majaribio hawana viwango vya kutisha kama ilivyojionyesha kwa waliopita,” alisema Katibu huyo. 
Tiboroha alisema mikakati yao ni kuwa na wachezaji ambao watawawezesha kutamba katika Soka la Afrika na kuwa klabu tishio barani humo, jambo ambalo halitawezekana kwa kusubiri wachezaji wa ‘mafungu’.
Baadhi ya wachezaji wa kigeni ambao waliwahi kutua nchini baada ya kuletwa na mawakala, lakini mwisho wa siku walichemka ni Mcameroon, Jama Mba (Yanga), Komal Bill Keita (Simba) na wengineo wengi.
Kwa sasa klabu za Ligi Kuu Bara zipo katika mchakato wa usajili wa wachezaji, zikianzia na makubaliano ya mikataba kabla ya kusaini fomu za usajili zitakazotolewa na TFF baadaye mwaka huu.
Chanzo:Bingwa

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini