KESI YA WAFUASI WA CHADEMA KUVAMIA POLISI YASOMWA LEO MAHAKAMANI

UPANDE wa Jamhuri katika kesi inayowakabili wafuasi watatu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) umedai mahakamani kwamba washtakiwa hao walikiuka amri halali ya Jeshi la Polisi baada ya kuvuka kizuizi kilichowekwa eneo la Makao Makuu ya  jeshi hilo.

Kadhalika, washtakiwa hao Ngaiza Kamugisha (28)  dereva, mkazi wa Vingunguti, Benito Mwapinga (30) Fundi nguo mkazi wa Mtoni kwa Azizi Ally na Eliasante Bugeji (51) Mhasibu wa CCBRT mkazi wa Komakoma Kinondoni, Dar es Salaam, wanadaiwa kukiuka amri halali iliyotolewa na Inspekta Zuhura ya kuwataka kutoweka eneo la ofisi hiyo.

Madai hayo yametolewa leo na Wakili wa Serikali Mkuu, Bernad Kongola wakati akiwasomea maelezo ya awali mbele ya Hakimu Mkazi Frank Moshi.

Kongola alidai kuwa Septemba 18, mwaka huu katika makao makuu ya jeshi la Polisi, washtakiwa walizuiliwa kuingia eneo hilo lakini walikiuka amri hiyo na kuingia kwa jinai.

Ilidaiwa kuwa mshtakiwa wa tatu, alitoa lugha chafu na matusi kwa Inspekta Zuhura iliyosababisha uvunjifu wa amani.

Washtakiwa walikana maelezo hayo.

Hakimu Moshi alisema kesi hiyo itasikilizwa Septemba 22 na 23, mwaka huu ushahidi wa upande wa Jamhuri.

Katika kesi ya msingi, ilidaiwa kuwa Septemba 18,mwaka huu, washtakiwa waliingia kinyume na sheria ndani ya Makao Makuu ya Jeshi la Polisi kwa hali ya fujo.

Alidai tarehe na siku ya tukio la kwanza washtakiwa walikataa kutii amri ya halali ya kutawanyika eneo la makao hayo iliyotolewa na  Inspeta Zuhura, ambaye alitoa amri hiyo baada ya kuruhusiwa na viongozi wake.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini