Wauza unga watumia utashi kukwepa mkono wa Dola kuuza dawa za kulevya


TATIZO la kuwepo na dawa za kulevya nchini bado ni kubwa na ukubwa uliopo imebainika kuwa haulingani na kiwango cha juhudi za kudhibiti tatizo hilo miongoni mwa wanajamii huku wauzaji wakiendelea kutumia mbinu mbadala kwa lengo la kufanikisha biashara hiyo.
FikraPevu imefahamishwa kuwa licha ya Jeshi la Polisi kupiga vita dawa hizo kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola pamoja na viongozi wa madhehebu ya dini biashara hiyo bado inaendelea kushamiri katika maeneo mbalimbali nchini hususani mikoa ya Dar es Salaam na Kanda ya Kaskazini wakitaka kupata utajiri wa haraka.
Wakiongea kwa nyakati tofauti na FikraPevu baadhi ya wananchi wa jiji la Tanga wamesema kuwa, matumizi ya dawa za kulevya kwa sasa ni tatizo sugu nchini ukiwemo mkoa huo na kwamba kwa sasa hali hiyo imekuwa kwa kasi kutokana na magari yanayofanya safari katika mikoa ya Kilimanjaro na Arusha kutumiwa kusafirisha dawa hizo bila kukamatwa na Polisi.
Walipoulizwa kwanini wanafikiri biashara hiyo imeshamiri zaidi katika maeneo mengi nchini, wamesema biashara hiyo inakuwa kutokana na kuhusisha watu wenye fedha nyingi na miongoni mwao ni viongozi wa juu serikalini na hivyo zoezi la kukomesha biashara hiyo haliwezi kufanikiwa.
Wakazi wa jiji la Dar es Salaam wameeleza kuwa pamoja na kuwepo kwa Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya biashara hiyo inaendelea kufanyika bila wahusika kukamatwa baada ya wengi wao kuhusishwa na biashara hiyo.
Mmoja wa wakazi hao, Andrew Hamza (25) mkazi wa Manzese na mwendesha Bajaji jijini humo ameitaka serikali kufanya mabadiliko ya sheria ya dawa za kulevya na kuanzisha Mahakama maalumu ya kushughulikia wahalifu wa dawa hizo ili kuendana na majira kwani nguvu inayotumika kudhibiti wahalifu hao hailingani na kile kinachotendeka na kwamba vijana ndio wanaoathirika zaidi.
“Vijana tunaoendesha Bajaji tunakutana na vitu vingi, unaweza kumwambia mteja kumpeleka mahali flani kiasi kikubwa cha hela lakini hajali anaitoa tena wakati ukimsikiliza akiongea na simu unajua kabisa kwamba hapa kuna dili la dawa za kulevya, tena anakupa mashariti makubwa kweli kwahiyo serikali ikawabana wanaoagiza itasaidia kwa kiasi kikubwa kukabiliana na hili tatizo” aliieleza FikraPevu.
Baadhi ya wakazi wa Kijitonyama wanasema zipo mbinu mpya za kutambua sehemu inayouzwa dawa hizo “Ukipita majira ya saa mbili hadi saa tano asubuhi katika mitaa hii (Karibu na barabara ya Afrika sana-Mabatini) ukiona akina mama wamekaa tu bila kazi au vijana alafu wamechoka choka alfu uone mfuko meusi umening’inizwa juu au raba jua hapo ndio penyewe, lazima wawe na mzigo wa bangi au gomba (mirungi)”.
Amesema ni wakati mwafaka kwa Bunge na serikali kuona uzito wa tatizo la dawa za kulevya kutokana na ukweli kwamba katika miaka ya karibuni tatizo hilo limeongezeka kwa kasi kubwa hali inayosababisha athari kubwa za kiuchumi.
Ripoti mpya ya hivi karibuni ya Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupambana na Mihadarati na Uhalifu imetamka wazi kwamba Tanzania ni kinara wa kupitisha dawa hizo katika nchi za Afrika Mashariki, na mkoa wa Tanga ulitanjwa kuwa ndio kiini cha mpaka unaotumiwa na wahalifu kusafirisha madawa hayo.
Tangu mwaka 2006, Rais Kikwete, alipotangaza vita dhidi ya wauzaji dawa za kulevya kumewahi kuripotiwa mzozo miongoni mwa viongozi wa dini, baada ya Rais Kikwete kueleza kuwa, baadhi yao wanahusika na biashara hiyo.
Kauli yake iliwafanya viongozi wakuu wa dini nchini kumtaka awataje viongozi hao lakini kwa upande mwingine, baadhi ya wafanyabiashara wa dawa hizo walikamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere, wakienda nchi jirani wakiwa wamezihifadhi katika sehemu za siri ili zisikamatwe huku takribani vijana 300 wakiripotiwa kutumikia kifungo katika mataifa ya China na Brazili kwa tuhuma za kukutwa na dawa hizo.
Viwanja vya Ndege
Jeshi la Polisi (kitengo cha) Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) mara kwa mara limekaririwa naFikraPevu likithibitisha kukamata raia mbalimbali wa kigeni kutoka mataifa ya nje wakiwa na gramu nyingi za dawa kulevya aina ya cocaine, Mirungi, na Bangi huku wengi wao wakiendelea kutesa mitaani na katika mataifa yao bila wasiwasi.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya Nchini, Kamanda, Godfrey Nzowa, anasema juhudi za kupamba na kundi hilo bado zinaendelea ambapo amekiri kuwepo kwa mbinu nyingine mpya zinazotumiwa na wahalifu kusafirisha na kuuza dawa hizo nchini na kwamba wanazijua.
“Hapa nchini hakuna sehemu inayotengenezwa madawa haya lakini uchunguzi unaonyesha kuwa yanatoka nje Cocein na dawa nyingine tukiachilia mbali mirungi na bangi ambayo inatapikana katika baadhi ya maeneo nchini”.
Kumekuwepo na kilio cha muda mrefu kuhusu tatizo hilo ikiwemo taarifa zinazotolewa na raia wema kuhusu wafanyabiashara hao ambao hadi leo asilimia kubwa ya watu hao wanaendelea kujineemesha kupitia biashara hiyo.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini