Kuhusu jamaa kumchoma mshale askari polisi





WATU wanne wamefikishwa mahakamani kwa mashtaka ya kuua ng’ombe 151 wenye thamni ya Sh milioni 60.4, mali ya mfugaji, Shabani Kidaini.


Watu hao, wote wakazi wa Turiani wilayani Mvomero mkoa wa Morogoro, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa huo.


Waliopandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka hayo na wakili wa Serikali, Teodora Mlelwa, mbele ya hakimu Agripina Kimaze, aliwataja washtakiwa hao ni Ally Ramadhani (64), Mussa Salumu (46), Mathew Daniael (46) na Imanuel Dismas (42) .


Mwanasheria huyo wa serikali alidai kuwa washtakiwa hao bila kibali halali huku wakijua kufanya hivyo ni kosa waliwaua ng’ombe hao kwa kuwakatakata na mapanga sehemu mbalimbali za miili yao. Washtakiwa hao kwa pamoja walikana mashtaka hayo na kurudishwa rumande baada ya kushindwa kukamilisha masharti ya dhamana zao.


Mahakama hiyo iliwataka kila mmoja kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya Sh milioni 15. Kesi hiyo itatajwa tena Januari 7, 2016 ambapo upelelezi bado unaendelea.


Katika hatua nyingine, Michael Kityanga (54) mkazi wa kijiji cha Msangalilo, Turiani wilayani Mvomero alipandishwa kizimbani katika mahakama hiyo mbele ya hakimu Regina Futakamba, kujibu mashtaka matatu yaliyokuwa yakimkabili. Mashitaka hayo ni kumjeruhi askari, kupora silaha ya askari na kuharibu mali ambayo ni gari la polisi.


Katika mashtaka ya kwanza, mwendesha mashtaka ambaye ni mwanasheria wa Serikali, Veronica Chacha alidai kuwa mshtakiwa huyo alitenda kosa hilo Desemba 13 , mwaka huu mwaka huu katika kijiji cha Dihinda, Turiani, wilaya ya Mvomero.


Mwanasheria huyo alidai kuwa mshtakiwa huyo aliiba bunduki ya kufyatulia mabomu ya machozi, ikiwa na mabomu ya machozi 10, mali ya Jeshi la Polisi Tanzania. Alidai kuwa kabla ya kuiba bunduki hiyo, alimjeruhi askari aliyekuwa akiitumia, Konstebo Peter wa Kituo cha Polisi Dakawa kwa kumkatakata kwa panga na kumchoma mshale.


Katika shtaka la pili, mshitakiwa huyo anadaiwa kuwa alimjeruhi askari polisi, sajini wa upelelezi Mkaze kwa kumchoma mshale mbavuni. Katika mashtaka ya tatu, mshtakiwa huyo alidaiwa kuharibu mali ambayo ni gari la polisi aina ya Toyota Land Cruiser lenye namba PT 0723 kwa kuvunja vioo na mlango wa gari hilo.


Mshtakiwa huyo alikana mashtaka yote na kurudishwa rumande kwa kuwa kesi hiyo kisheria haina dhamana. Kesi hiyo itatajwa tena Januari 6, 2016 na upelelezi bado unaendelea

ASANTE KWA KUTEMBELEA MTANDAO WETU!!

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini