MCHEPUKO Unavyoweza Kuua!

HABARI wapendwa wasomaji wa safu hii, tunaojumuika pamoja kila wiki katika kutazama moja ya filamu za nyumbani, ili kuweza kuelezana hili na lile, lenye kulenga kuboresha zaidi kazi zetu ili ziweze kufikia viwango vya kimataifa kama walivyo wenzetu.

Leo tunayo filamu iitwayo Big Surprise, ambayo waigizaji wakuu ni Jennifer Kyaka ‘Odama’, Mohamed Fungafunga ‘Jenguo’ na Gabo Ziganda, kijana ambaye nimewahi kutabiri kuwa atakuwa mmoja kati ya waigizaji wazuri siku zijazo, endapo ataendeleza umakini wake alionao sasa.

Ni filamu nzuri, inayoonyesha jinsi gani dunia ilivyogubikwa na maajabu kila kukicha, kwani unamuamini mtu, lakini kinachotokea kinakushangaza. Gabo ni mume wa Odama wakiwa wamejaaliwa kuzaa mtoto mmoja, Beatrice. Lakini anakutana na habari kuwa mkewe ni mchepuko, mwenye tabia ya kutembea na watoto wadogo.

Odama anabisha sana suala hilo, lakini siku moja anamfumania akiwa na kiserengeti boy wake. Baada ya hapo, mumewe anaamua kumnyamazia bila kusema lolote, kitu ambacho kinamuuma sana Odama, kwani aliona ni adhabu kubwa mno, ni bora kama angefanywa chochote kuliko kunyamaziwa kama hivyo.

Hali hiyo ya kutojua hatima yake inamsababisha afikie uamuzi wa kunywa sumu na kufa. Kimsingi ni filamu nzuri yenye mafunzo kibao, lakini ina makosa mengi ya kiufundi yanayoondoa ubora uliokusudiwa. Kwanza nimpongeze sana mtoto Beatrice, amecheza vizuri sana eneo lake na hakika, huyu ni hazina kubwa ijayo.

Kuna siku rafiki wa Gabo alimweleza kuwa mke wake hakuwa mwaminifu, lakini siku ambayo alipanga kumfanyia surprise mkewe kwa kumsamehe na kumpa zawadi siku ya kumbukumbu yake ya kuzaliwa, ndiye huyohuyo aliyesifu mpango huo badala ya kubakia kwenye msimamo wake.

Baada ya Odama kujiua, Gabo na marafiki zake wanaamua kuupeleka mwili wake nyumbani kwao kijijini, ambako wazazi wake (Jenguo) anaukataa kwa maelezo kuwa haamini kama mwanaye alijiua, yeye anadhani aliuawa. Isitoshe, tangu aondoke kijijini, hawakuwahi kusikia kama aliolewa na alikuwa na mtoto.

Msafara wa kina Gabo kijijini ulifuata utaratibu kwa kwenda kwanza kwa mwenyekiti wa mtaa kujitambulisha, lakini simulizi inaonekana kuwa na kasoro, unapogundua kwamba kwa muda wa siku nne ambao gari lenye maiti lilikaa kijijini pale, hakuna hata jirani mmoja aliyekuja na kuwauliza au kushangaa kulikoni!

Katika jamii ya Kitanzania, jambo hili kidogo lina utata, kwani kwa wanaoishi vijijini, ni wepesi kujumuika pamoja kwenye matatizo makubwa hasa misiba. Hatimaye siku ya nne mzee Fungafunga anakubali kuuchukua mwili wa mwanaye, lakini ajabu nyingine, ni vijana watatu hivi ndiyo wanaushusha mwili huo garini.

Kwa maisha ya vijijini, siku hiyo ilipaswa kuwa na watu wengi, hasa kwa kuwa Odama ni mwenzao na tukio hilo ni kubwa na la kustaajabisha.

Baada ya mazishi ya mkewe, Gabo kidogo anapatwa na matatizo ya akili, akibeba pochi ya mkewe kazini na kufanya vituko vya hapa na pale hadi jamaa zake wanapomuitia mchungaji kwa maombezi. Lakini katika uchizi wake, unashangaa kwamba anavaa vizuri, anakwenda kazini na hata kuzijua taratibu zote za maisha yake ya kila siku.

Ungetegemea mtu aliyerukwa na akili kupotea njia, kutojua lolote na hata kuchanganya mavazi. Kwa ujumla ni filamu nzuri ambayo kama dosari hizi zingeondolewa ingekuwa bora zaidi. Sifa za pekee ni kwa mtoto Beatrice, kwani ametimiza majukumu yake vizuri!

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini