Waziri NYALANDU Afunguka Kuhusu Kuchafuliwa MItandaoni!

Mbunge wa Singida Kaskazini aliyemaliza muda wake, Lazaro Nyalandu, amewataka wagombea wenzake kuacha kucheza rafu na kumchafua na badala yake waendeshe siasa safi kwa maendeleo ya wananchi.

Amesema vitendo vya hujuma vinavyofanywa na baadhi ya washindani wake wanaowania ubunge kwenye jimbo hilo kwa kuandaa makundi ya kumzomea, haviwezi kuleta tija kwa wapigakura.

Nyalandu ambaye pia ni Waziri wa Maliasili na Utalii, alisema ni muhimu kwa wagombea wote kufuata kanuni na taratibu za uchaguzi ili mwisho wa siku apatikane mgombea bora atakayewasambaratisha wapinzani.

Alikuwa akizungumza na waandishi wa habari katika Ofisi za CCM Mkoa wa Singida jana kuhusiana na mchakato wa uchaguzi ndani ya Chama unavyoendelea.

Alisema baadhi ya wagombea wamekuwa wakiacha kueleza sera za mikakati na badala yake kumpaka matope.

Hata hivyo, alisema kamwe hatakata tamaa na badala yake ataendelea kuwafikia wana-CCM na kueleza mikakati yake ya kuwatumikia na kwamba mengi aliyoahidi ameyatekeleza kwa mafanikio makubwa.

“Siasa safi ndiyo zinazotoa na kujenga wagombea makini, bora na wenye ushindani dhidi ya upinzani. Siasa za kuandaa watu wachache ili wamzome Nyalandu, haziwezi kuwa na tija kwa maendeleo ya wananchi wetu,” alisema.

Aliongeza: “Tushindane kwa hoja na mikakati ya maendeleo kwa wapigakura wetu ili mwisho wa siku twende kuwakabili wapinzani tukiwa kamili na wamoja ili kusaka ushindi wa kishindo.”

Alisema kitendo cha kuwashikisha mabango yenye picha zake wanafunzi na kuwapiga picha na kuweka kwenye mitandao, kamwe hakiwezi kumchafua ama kumkatisha tamaa badala yake ataendelea kusonga mbele na kuwa bora zaidi katika kunadi sera zake mbele ya wapigakura.

Kauli hiyo ya Nyalandu imetokana na baadhi ya watu wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa wapinzani wake, kumzomea na kupiga kelele wakati anapojieleza kwa wananchi kwa lengo la kumvuruga.

Hata hivyo, alisema anafahamu mambo hayo hujitokeza kwenye siasa na bado ana dhamira na uwezo wa kuwatumikia wapigakura wa Singida Kaskazini.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini