Wageni 2,000 matatani kwa kujiandikisha BVR



Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji nchini, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Abbas Irovya akizungumza na waandishi wa habari na maofisa Uhamiaji kutoka wilaya za Dar es Salaam jana kuhusu mambo mbalimbali yaliyotekelezwa na idara hiyo ikiwemo kukamata zaidi ya raia wa kigeni 2000 wakiwa na kadi za kujiandikisha kupiga kura. (Picha na Fadhili Akida).

IDARA ya Uhamiaji nchini imetoa onyo kwa raia wa kigeni watakaobainika kuwa na vitambulisho vya kupigakura baada ya kubaini raia hao zaidi ya 2,000 kuwa na vitambulisho hivyo katika msako unaofanywa na maofisa wao kwenye miji iliyo mipakani hapa nchini.

Idara hiyo imesema tayari imeshaanza kuwachukulia hatua za kisheria raia hao ikiwa ni pamoja na kuwanyang’anya vitambulisho hivyo, kuwaondoa nchini baadhi na wengine kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.

Mikoa ambayo raia hao wamebainika kujiandikisha kwenye daftari hilo na idadi yake kwenye mabano ni pamoja na Kagera (708), Mara (619), Tanga (348), Kigoma (254), Rukwa (13) na Kilimanjaro (12).

Mikoa mingine ni Ruvuma (9), Geita (6), Shinyanga (7), Mtwara (3), Pwani (2), Dar es Salaam (65), Mbeya na Morogoro mmoja kila mkoa. Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji nchini, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Abbas Irovya alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa, maofisa wa Idara hiyo wanaendelea na uchunguzi na watakapowabaini wengine hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Aidha alisema ni kosa kisheria kwa raia yeyote wa kigeni kujiandikisha ili apate kitambulisho cha kupiga kura na hivyo kuwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa kuwafichua raia hao.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini