MWAKYEMBE: LOWASSA Ndiye Richmond...Aliamua Kujiuzulu Uwaziri ili Kukwepa Aibu Kama Ingejulikana!

MJUMBE wa timu ya kampeni ya CCM, Dk Harrison Mwakyembe, amesema sakata la kashfa ya Richmond, haliwezi kuachwa kuzungumzwa na wanaCCM kwa kuwa mgombea urais kupitia Chadema, Edward Lowassa ameanza kusingizia watu wengine kuhusika na kashfa hiyo, jambo ambalo alisema haliwezi kuachwa lipotee bila kujibiwa.

Aliyasema hayo alipokuwa akiwahutubia wakazi wa Ubungo jana, mkutano uliokwenda sambamba na kumnadi mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM, Dk Didas Massaburi.
“Unaposema kuna wakubwa juu waliamuru Mkataba wa Richmond usivunjwe maana yake unamsema Rais wa nchi.

"Katika suala lile hakuna rais wala nani, mhusika mkuu ni Lowassa na alifanya hivyo kwa uroho tu wa kutaka kujipatia fedha na upo ushahidi wa maboksi mawili.
“Tulimpa masharti mawili; Kwanza ajipime kutokana na ushahidi uliopatikana wa yeye kushiriki. Pili ilikuwa ni kwa Bunge kuthibitisha ushiriki wake endapo angegoma.
"Alichofanya ni kuamua kujiuzulu ili kukwepa aibu. Sasa katika hili rais anatokea wapi au anaposema alionewa ni katika lipi?” Alihoji.

Akizungumzia kutofuatana na Dk Magufuli katika mikutano yake kuzungumzia kashfa ya Richmond na kuachia makada wengine kuzungumzia suala hilo, Dk Mwakyembe alisema ni kutokana na wajumbe 32 wa Kamati ya Kampeni kuwa na majukumu katika maeneo mbalimbali nchini.

“Wale wajumbe 32 tumegawanyika katika maeneo mbalimbali, na kila mtu anaonana na wananchi kwa njia na staili tofauti lakini lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa CCM inaibuka na ushindi wa kishindo. Hata kama wajumbe wote 32 tukifuatana na Dk Magufuli hatuwezi kuzungumza wote kutokana na muda,” alisema.

Akimnadi Dk Masaburi, Dk Mwakyembe ambaye pia ni mgombea ubunge wa Jimbo la Kyela na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, alisema mgombea huyo wa ubunge katika Jimbo la Ubungo kupitia CCM ni aina ya wachapakazi ambao wanahitajika katika uongozi ujao wa Dk Magufuli katika kuwaletea wananchi maendeleo.

“Jimbo la Ubungo ni jimbo la kimkakati kutokana na umuhimu wake. Kwanza ni Jimbo la viwanda, pili ni lango la Jiji na hivyo ni sura ya Dar es Salaam, lakini tatu ni Jimbo la Elimu ya Juu kutokana na kuwepo kwa Chuo Kikuu na Chuo cha Usafirishaji. Dk Masaburi ni aina ya mbunge anayehitajika kuliongoza ili kulifanya Taifa kulitendea haki,” alisema.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini