DARASA LA WAKUBWA:NINI CHA KUFANYA IKIWA WAZAZI NA NDUGU ZAKO WANAMCHUKIA MPENZI WAKO??

Je, upo kwenye uhusiano wa kimapenzi, unampenda sana mume, mke, mchumba au mpenzi uliyenaye lakini wazazi au ndugu zako wanamchukia na kila siku wanampiga vita?
Mada ya leo ni kwa ajili ya wewe msomaji wangu ambaye upo kwenye mazingira kama haya ya wazazi au ndugu kumkataa umpendaye kwa sababu ambazo wanazijua leo. Kwa ambao wamewahi kupitia changamoto hii au bado wapo ndani yake, watakuwa wanaelewa vizuri ugumu uliopo linapokuja suala kama hili.
Wazazi wako wamekuzaa na kukulea tangu ukiwa mdogo mpaka umekuwa mkubwa, umempata umpendaye lakini wao wanamkataa na kukwambia unatakiwa kuchagua moja, wao (wazazi) au huyo unayempenda. Utachukua uamuzi gani? Utamuacha kwa sababu wazazi hawampendi? Utakubali kuwadharau wazazi wako na kuendelea naye?
Bila shaka kila mmoja atakuwa na jibu lake tofauti, hata mimi ukiniuliza nitakuwa na jibu langu lakini tunachokihitaji hapa, ni kujadiliana, kupanuana mawazo, kupeana uzoefu ili mwisho kila mmoja awe na uwezo wa kuivuka changamoto hii kwa sababu hata kama bado haijakukuta, huenda ipo siku na wewe yatakutokea.
MFANO HAI
Hebu soma ushuhuda wa msomaji wangu mmoja ambaye yupo kwenye hali mbaya na anahitaji ushauri:
“Mimi ni mwanaume mwenye umri wa miaka 42, nilioa miaka kumi iliyopita na tumejaliwa kupata watoto wawili. Tatizo linalonisumbua na kuniweka njia panda, mke wangu anawachukia sana wazazi wangu na ndugu wote kutoka upande wangu.“Wazazi wangu wamekuja mjini kwa zaidi ya miezi miwili sasa kwa ajili ya matibabu lakini huwezi kuamini, mke wangu anawachukia kiasi kwamba hata salamu kwake ni mtihani. Anawadharau, wanapishana ndani kama wake wenza, anazungumza maneno machafu dhidi yao ambayo mengine nayasikia, hawapi matunzo mazuri, anawanyanyasa na kibaya anawafundisha mpaka wanangu kuwadharau babu na bibi.
“Hali hiyo imesababisha wazazi nao waanze kumchukia sana, wananiambia nimekosea kuchagua mke na wananitolea maneno makali ambayo mengine hayaandikiki. Nipo njia panda, sijui niamue nini, bado nampenda mke wangu lakini mambo anayoyafanya yamesababisha mapenzi yangu kwake yapungue mpaka nafikiria kumpa talaka ili kuwafurahisha wazazi wangu. Naomba ushauri, nifanyeje?”
Amehitimisha msomaji wangu huyu, bila shaka umemuelewa. Najua huyu ni mmoja tu lakini wapo wengi ambao wanatokewa na visa kama hivi. Naomba tujadiliane pamoja, ungekuwa ni wewe kwenye nafasi ya msomaji huyu, ungefanya nini? Kama ungepewa kazi ya kumshauri, ungemwambia nini?
TAFUTA CHANZO CHA TATIZO

Hakuna chuki ambayo huwa haina chanzo. Kama mumeo, mkeo anawachukia ndugu zako, jambo la kwanza ambalo unatakiwa kulijua, ni kwamba lazima kuna chanzo kilichosababisha hali hiyo. Na kama yalivyo matatizo mengine yote, huwezi kupata muafaka kama hujakijua chanzo.
Wengi hushindwa kutumia busara katika kutafuta chanzo. Yawezekana umpendaye ndiyo chanzo ila kwa sababu ya mapenzi yako kwake, unaukataa ukweli na kumtetea.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini