MCHINA AKAMATWA HUKO PWANI BAADA YA KUMTEKA MWENZAKE, AKUTWA NA RISASI 300


JESHI la Polisi mkoani Pwani linamshikilia raia wa nchi ya China We Sheng (39) mkazi wa Mbagala jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za kumteka nyara Mkurugenzi wa Kiwanda cha Kutengeneza Viatu vya Plastiki (Yeboyebo), Li Cheng Weng (54) baada ya kumtishia kwa silaha.Mtuhumiwa huyo alitoa sharti na kumtaka mlalamikaji atoe fedha kiasi cha dola za Kimarekani 350,000 (sawa na Sh milioni 584.5) ili amwachie huru.


Akizungumza ofisini kwake mjini Kibaha, Kamanda wa Polisi Mkoani Pwani, Ulrich Matei alisema tukio hilo lilitokea Oktoba 19 mwaka huu majira ya saa 4.00 usiku wilayani Mkuranga.


Kamanda Matei alisema kuwa baada ya kupekuliwa kwenye gari lake aina ya Toyota Land Cruiser lenye namba za usajili T 554 BAJ alikutwa na bunduki aina ya Short gun namba 006085010, risasi 98 na visu viwili.


Kwa mujibu wa Kamanda Matei, Polisi walikwenda kupekua nyumbani kwa kijana huyo wakakuta nyaraka zinazoonesha kuwa, amewahi kumiliki risasi 300, hivyo haijafahamika risasi 202 amezitumia wapi.


Amesema, Ubalozi wa China umewafahamisha polisi kuwa, mtuhumiwa huyo alikuwa akishiriki kufanya uhalifu nchini humo.


Kamanda Matei alisema , polisi wanawasiliana na wenzao wa Shirika la Polisi la Kimataifa (Interpol) ili kupata taarifa zaidi kuhusu kijana huyo.


Katika tukio lingine, watu watatu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wamekamatwa wakiwa na bunduki aina ya Short gun yenye namba 07019302 ikiwa na risasi nane.


Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mohamed Kalipa (20) dereva wa Bajaji mkazi wa Mbagala Rangi Tatu, Salum Shekivui (20) mkazi wa Buza na Seuli Lucas (18) mkazi wa Mbagala Rangi Tatu jijini Dar es Salaam.


Kamanda Matei alisema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa Oktoba 20 mwaka huu majira ya saa 2:30 Mlandizi wilaya ya Kibaha.


“Mbali ya silaha pia walikutwa na fedha taslimu kiasi cha Shi milioni 6,611,800, vocha mbalimbali za simu zenye thamani ya Sh milioni 2,185,500 na simu za mkononi sita za aina mbalimbali ambazo thamani yake bado hazijafahamika,” alisema Kamanda Matei.


Aidha alisema kuwa watuhumiwa hao wanadaiwa kuwa walifanya tukio la unyang'anyi wa kutumia silaha katika kijiji cha Mbwewe wilaya ya Bagamoyo kwenye duka la Twaha Mbuta, Oktoba 19 saa 1:30 usiku na kupora kiasi cha Sh milioni 30.


“Baada ya kukamatwa walimtaja mtuhumiwa mwenzao ambaye walikuwa wakishirikiana naye Samwel Joseph mkazi wa Kongowe, Kibaha ambapo baada ya upekuzi walimkuta na risasi sita za Short gun ambazo alikuwa akizimiliki bila ya kibali. Hata hivyo mtuhumiwa huyo alitoroka,” alisema Kamanda Matei.


Katika tukio lingine watu wawili walikamatwa kwa tuhuma za wizi wa ng'ombe 61 wenye thamani ya Sh milioni 27.4 mali ya Keke Furaha (37) kwa kutumia silaha aina ya sime.


Alibainisha kuwa tukio hilo limetokea Oktoba Mosi mwaka huu majira ya saa 5.00 asubuhi eneo la Lulenge kata ya Ubena wilayani Bagamoyo.

 Watuhumiwa katika tukio hilo ni Sadala Lupoto (25) mkazi wa Kimamba Kilosa na Luseky Sogoyo (25), na juhudi za kuwatafuta ng'ombe wengine 39 zinaendelea.

Na John Gagarini

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini