Aibu! Askari Polisi Mbaroni akidaiwa Kubaka Mwanafunzi wa Kidato cha Kwanza Shinyanga

Askari polisi wa kituo kikuu cha Shinyanga aliyefahamika kwa jina moja la Alex, amewekwa korokoroni akituhumiwa kumbaka mwanafunzi wa kidato cha kwanza , mkazi wa kata ya Ngokolo mjini hapa na kumsababishia maumivu makali sehemu za siri.



Kamanda wa polisi mkoani Shinyanga, Justus Kamugisha, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo huku akisema jeshi hilo linaendelea kufanya uchunguzi ili kubaini ukweli kamili, akigoma kutaja jina kamili la mtuhumiwa huyo hadi hapo uchunguzi utakapokamilika.
 
“Tunaendelea kufanya uchunguzi, lakini sina haja ya kutaja jina lake kwa sasa hadi hapo tutakapothibitisha hilo,” alisema kamanda Kamugisha.
 
Akizungumza na mwandishi wetu jana, mama mdogo wa mwanafunzi huyo, Neema Elisha, alisema tukio hilo lilitokea Januari 4, mwaka huu, saa 8:00 usiku, wakati binti huyo alipotoka nje kujisaidia na kukutana na polisi huyo aliyemvutia ndani mwake na kutekeleza unyama wake.
 
Elisha alisema aliposhituka muda huo, hakuweza kumuona binti yake kitandani huku mlango ukiwa wazi na alipomfuatilia hakuweza kumkuta chooni, hivyo aliporudi kusubiri alimuona anatokea kwa polisi huyo akiwa mnyonge.
 
“Siku hiyo mume wangu hakuwapo, nililala na binti yangu kitanda kimoja lakini ghafla sikumuona mtoto kitandani, nilipotoka nje kumuangaza sikumuona na baadaye nikamuona anatokea akiwa mnyonge,” alisema Elisha.
 
Alisema alipomhoji hakuweza kumwambia hadi alipomtisha ndipo aliposema alipoenda kujisaidia alivutwa ndani na polisi huyo na kumlazimisha kufanya naye mapenzi kwa nguvu huku akimtisha na kumziba mdomo.
 
Hata hivyo, mwanafunzi huyo alisema askari polisi huyo ambaye ni mpangaji katika nyumba hiyo anayoishi mama yake mdogo, alikuwa na kawaida ya kumtongoza kila wakati na kumkatalia, lakini siku hiyo ndipo alipopata nafasi ya kumbaka.
 
“Nilisikia maumivu makali wakati ananiingilia kimwili, kwani wakati anafanya hivyo alinizidi nguvu huku akiniziba mdomo ili nisiweze kufurukuta,” alisema mwanafunzi huyo.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini