Wanafunzi 48 wasichana wa shule ya sekondari ya Muungano wanusurika Kufa baada ya bweni lao Kuteketea kwa moto

Wanafunzi 48 wasichana wa kidato cha kwanza wa shule ya sekondari ya vipaji maalum ya Muungano wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro wamenusurika kifo baada ya bweni lao kuteketea kwa moto na vifaa vyao vyote.
 
Mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo ya wananchi Mh Zawadiel Maruchu amesema, moto huo ulianza kwenye bweni hilo kuanzia saa moja usiku wakati wanafunzi wakijiandaa kupata chakula lakini hamna aliyejeruhiwa.
 
Mh Maruchu amevipongeza vyombo vya ulinzi, zima moto na wananchi kwa ushirikiano wao mkubwa uliofanikisha kuzimwa kwa moto huo ambao umetekeza vifaa vyote ingawa kuna mabaki kidogo ya nguo.
 
Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Moshi Bw Flugence Mponji amesema, wanafunzi wa kidato hicho wamerudishwa nyumbani kwao kwa wiki moja wakati serikali inafanya juhudi za haraka kuwatafutia malazi.
 
Wanafunzi wa shule hiyo wameiomba serikali iimarishe ulinzi na kuweka uzio wa shule na kufanya uchunguzi wa kina juu ya tukio hilo ambalo limeacha maswali mengi miongoni mwa wananchi wa kata ya kilema kusini.
 
Wazazi wa wanafunzi hao wameiomba serikali iweke miundo mbinu yenye hadhi ya shule hiyo kuwa ya bweni ya wasichana wa vipaji maalum kuliko hali ilivyo sasa ambayo mazingira yake ni hatarishi.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini