SAKALA LA ESCROW: Chenge na Ngeleja waachia vyeo bungeni Andrew Chenge

Andrew ChengeWENYEVITI wa Kamati za Kudumu za Bunge, waliopendekezwa kuwajibishwa na Bunge hilo katika sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow, wamejiuzulu nyadhifa zao.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Spika Anne Makinda aliwaambia waandishi wa habari katika Ofisi ndogo ya Bunge, waliotaka kujua hatima ya wenyeviti hao, kuwa hawapo tena katika nafasi zao baada ya kujiuzulu.
“Wenyeviti hao kwa ninavyojua mimi wamejiuzulu, kama ambavyo azimio lilivyotaka, kama wapo hizo taarifa mimi sina na sijui kinachoendelea, nawaambia mimi wameshajiuzulu,” alisema Spika Makinda.
Makinda alisema wenyeviti hao, ambao ni wa Kamati ya Nishati na Madini, Victor Mwambalaswa, wa Katiba, Sheria na Utawala William Ngeleja na Andrew Chenge wa Kamati ya Bajeti, hawaendelei tena na nafasi zao, kupisha viongozi wengine kuchaguliwa ndani ya kamati husika.
Hata hivyo, Makinda alipoulizwa kama wenyeviti hao kama wamejiuzulu rasmi kwa barua na kama yeye amezipokea lini, alisema viongozi hao ni wa kamati na hivyo wamewajibika katika kamati zao.
“Mimi ndiye Spika, nasema wamejiuzulu… msiniulize barua zao wala nini, heshima ya mtu ni kujiuzulu mwenyewe bwana na wao wamefanya hivyo,” alisema Spika Makinda.
Katika Azimio namba tatu la Bunge katika majadiliano ya sakata hilo, Bunge lilielekeza kuwa kamati husika za kudumu za Bunge, zichukue hatua za haraka na kwa vyovyote vile kabla ya mkutano wa 18 wa Bunge, kuwavua nyadhifa zao wenyeviti tajwa wa kamati husika za kudumu za Bunge.
Utekelezaji wa azimio hilo, unakuja baada ya Serikali kutekeleza maagizo ya Bunge hilo kwa kuwawajibisha baadhi ya viongozi wake, waliotajwa katika ripoti hiyo.
Chenge ambaye ni Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), alitajwa katika ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuwa aliwekewa Sh bilioni 1.6 katika akaunti yake binafsi na Ngejela ambaye ni Mbunge wa Sengerema (CCM) aliingiziwa Sh milioni 40.4 kwenye akaunti.
Waliingiziwa fedha hizo na mmiliki wa Kampuni ya VIP Engineering & Marketing, James Rugemalira. Mwambalaswa ambaye pia ni Mbunge wa Lupa (CCM), ametajwa kuwa alikuwa Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Umeme nchini (TANESCO), ambayo Bunge liliazimia kuwa wajumbe wake wote wawajibishwe.
Katika utekelezaji wa maazimio hayo, Rais Jakaya Kikwete alimtaka Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka kupisha katika nafasi hiyo ili ateuliwe mtu mwingine na tayari Profesa huyo ameshapisha.
Profesa Tibaijuka aliingiziwa Sh bilioni 1.6 katika akaunti yake binafsi, kinyume na kanuni za maadili ya viongozi wa umma.
Rais Kikwete pia alimweka kiporo Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi amesimamishwa kazi kupisha uchunguzi wa tuhuma dhidi yake.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, alishajiuzulu.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini