TANESCO WAPEWA SIKU 7 WAUNGANISHE UMEME

WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ameitaka Bodi mpya ya Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kuliongoza shirika hilo kwa ufanisi na kuhakikisha kuwa mteja mpya anapoomba umeme anafungiwa ndani ya wiki moja.
Pia waziri huyo ameitaka bodi hiyo kuhakikisha kuwa shirika hilo linajitegemea na hivyo kupunguza utegemezi wa fedha kutoka serikalini.
Akizindua bodi hiyo mwishoni mwa wiki, Profesa Muhongo alielezea kukerwa na suala la wananchi kufungiwa umeme ndani ya siku 30 mara wanapopeleka maombi hayo Tanesco na hivyo kuiagiza bodi hiyo kulishughulikia suala hilo ili siku hizo zipungue.
“Bodi simamieni maombi ya kufungiwa umeme ambayo sasa yanaelezwa kushughulikiwa ndani ya siku 30, hii lazima ibadilike, Watanzania lazima wapewe umeme ndani ya wiki, zaidi ya hapo haikubaliki. “EWURA (Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji) waelezwe kuhusu suala hili ili kuona namna ya kupunguza hizi siku, sababu wao wanahusika katika suala la upangaji wa siku husika,” alisisitiza Profesa Muhongo.
Akizungumzia haja ya Tanesco kujitegemea kifedha, alisema kwa kipindi kirefu, serikali imekuwa inatoa fedha nyingi kuisaidia kutekeleza miradi katika maeneo ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme.
Hivyo alitaka bodi hiyo kuonesha jinsi itakavyolibadilisha Shirika ili misaada kutoka serikalini ipungue na ifike mahala shirika hilo lijitegemee.
Kuhusu madeni ambayo Tanesco inadai kutoka kwa Taasisi za Umma, binafsi na watu binafsi, Waziri Muhongo aliiagiza Bodi hiyo kulisimamia suala hilo na kuja na mkakati utakaoliwezesha shirika hilo kukusanya madeni hayo.
Alisema lengo la Serikali ni kuona shirika hilo linakusanya madeni kutoka kwa wadeni wake wakubwa na wadogo ili Shirika hilo nalo liweze kulipa madeni linalodaiwa na wadau wake.
Aidha, Profesa Muhongo ameiagiza bodi hiyo mpya kuhakikisha kuwa shirika hilo linashirikiana na sekta binafsi katika miradi yake ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji umeme ili kufanikisha lengo la serikali la kuzalisha umeme wa kiasi cha megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025.
Alieleza kuwa, kulingana na sera zilizopo, uendelezaji wa sekta ya umeme, unahitaji ushirikishwaji wa sekta binafsi kwa kuwa uwekezaji katika sekta hiyo unahitaji kiasi kikubwa cha fedha za kigeni, kiwango ambacho kinahitaji ushirikiano na sekta hizo.
Alisema Tanesco inapaswa kuonesha nia thabiti ya kuunga mkono juhudi za serikali za kukamilisha majadiliano na wawekezaji na waendelezaji wa miradi bila kuwakatisha tamaa.
Awali, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Masele aliieleza bodi hiyo kwamba serikali ina imani kuwa uzoefu na weledi wa Mwenyekiti na wajumbe wa bodi hiyo utasaidia katika kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya nishati ili sekta hiyo muhimu ichangie katika kuipeleka nchi kwenye uchumi wa kati.
Naibu waziri huyo aliwaasa wajumbe hao kuhakikisha kuwa taaluma walizonazo wanazitumia katika kuliboresha shirika hilo. Naye Mwenyekiti wa Bodi hiyo Dk Mighanda Manyahi alisema majukumu waliyokabidhiwa ya kuisimamia Tanesco ni makubwa, lakini kwa kutumia taaluma zao watahakikisha wanayatimiza ili kuhakikisha nchi inakuwa na umeme wa uhakika kwa kuwa nchi ina rasilimali za kutosha zinazowezesha kutimiza malengo hayo.
Mwenyekiti huyo wa Bodi ya Wakurugenzi wa Tanesco anaongoza wajumbe nane ambao ni Kissa Vivian Kilindu, Juma Mkobya, Dk Haji Semboja, Shaaban Kayungilo, Dk Mutesigwa Maingu, Boniface Muhegi, Felix Kibodya na Dk Nyamajeje Weggoro.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini