KILICHOKUJA MBELE YA KIFO CHA AJALI YA CARISTA, MKE WA BILIONEA ARUSHA








Stori: Joseph Ngilisho, ARUSHA/UWAZI
MAZISHI ya Carista Charles Makoi, 52, (pichani), ambaye alikuwa mke wa mfanyabiashara bilionea jijini hapa, Charles Makoi yamefanyika huku shilingi milioni 200 zikisemekana kuteketea kwa bajeti.
Mfanyabiashara maarufu jijini hapa, Patrick Ngiloi ambaye ni mmiliki wa vituo vya mafuta vya Kampuni ya Panone ndiye aliyekuwa mwenyekiti wa kamati ya mazishi hayo.

Kwa mujibu wa chanzo makini ndani ya kamati hiyo, siku ya kwanza tu baada ya kifo hicho, saa tatu mbele zilichangwa zaidi ya shilingi milioni 75 na baada ya hapo ziliendelea kuchangwa hadi kufikia lengo.
WACHANGAJI WAKUBWA
Chanzo kilisema kuwa, wachangaji wakubwa walikuwa wafanyabiashara wakubwa kutoka mikoa ya kaskazini mwa Tanzania, ikiwemo Arusha, Kilimanjaro na Tanga.“Wengi waliowahi kuchanga ni wafanyabiashara wa mikoa hiyo niliyokutajia. Lakini tulidhamiria bajeti iwe ya milioni mia mbili. Unajua shughuli ni shughuli siku zote.
“Tunaposema milioni mia mbili tulimaanisha kwa ajili ya kununulia vinywaji, kama bia, maji na soda. Pia vilinunuliwa vyakula mbalimbali, jeneza, sare na kuandaa mahali pa kukaa waombolezaji kutoka sehemu mbalimbali. Waombolezaji walikuwa wengi sana ndiyo maana bajeti ilikuwa kubwa.
“Kwa kweli tulikwenda sawasawa, hakuna mahali tulikwama. Ni bajeti ya aina yake hii,” kilisema chanzo hicho na kuomba hifadhi ya jina lake
WALIVYOSEMA WAOMBOLEZAJI
Baadhi ya waombolezaji walisikika wakiteta kuwa, bajeti hiyo ilitosha kufanya miradi kadhaa ya maendeleo kama kununua madawati, vyandarua mahospitalini na magari kwenye vituo vya afya.
“Mfano, nimesikia kwamba jeneza peke yake ni shilingi milioni saba, si unaweza kununua Toyota Vitz?” alihoji mwombolezaji mmoja na kujibiwa na mwenzake kwamba, mawazo kama hayo ni kuingilia uhuru wa familia ya marehemu.
“Marehemu alikuwa na gari zaidi ya Vitz, unaposema inaweza kununua Vitz unamaanisha nani sasa? Wakupe wewe ukanunue au ndugu yako? Huko ni kuingilia uhuru wa familia ya marehemu,” alihoji mwombolezaji mwingine.
MAZISHI YA AINA YAKE KIBOSHO
Baada ya msiba Arusha, msafara ulianza kuelekea Kibosho mkoani Kilimanjaro ambako marehemu alizikwa Ijumaa iliyopita nyumbani kwa familia hiyo, Sambani, Kibosho.Yalikuwa mazishi ya kwanza kwa idadi kubwa ya waombolezaji kutoka Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Mwanza, Dar es Salaam, Morogoro huku magari ya kifahari yakiwa mengi.
WAOMBOLEZAJI WALIACHA BIA
Wakati wa msiba huo uliokuwa maeneo ya Sakina jijini hapa, waombolezaji wanaopata ‘yale mambo’ walikunywa pombe mbalimbali zikiwemo bia na ilifika mahali walizikodolea macho kwa kinai kama si kulewa.
“Da! Hii balaa, hapa mtu usipojiangalia unaumbuka hivihivi unajiona, mimi bia basi tena, sasa nakwenda na maji kwanza,” alisikika akisema mmoja wa waombolezaji msibani siku ya kwanza.
MAKOI NI NANI?
Mume wa marehemu Carista, Charles Makoi anamiliki hoteli maarufu iliyopo jijini Arusha inayojulikana kwa jina la Aquiline (ghorofa 7), vituo vya mafuta Arusha na Moshi, maduka ya bidhaa mbalimbali jijini Dar, Morogoro, Kilimanjaro, Iringa na Tanga.
Anaishi kwenye nyumba kubwa ya kifahari iliyopo Sakina.
TUJIKUMBUSHE
Marehemu Carista alipata ajali Januari 5, mwaka huu baada ya gari alilokuwa akiendesha kutoka Moshi kwenda Arusha, Mitsubishi Pajero lenye namba za usajili T 930 AVZ kugongana uso kwa uso na basi aina ya Hino (Mrindoko Trans) lenye namba za usajili T 312 AVG maeneo ya Kikatiti, Arumeru, Arusha.
Carista Charles Makoi enzi za uhai wake.
Katika ajali hiyo, marehemu alifariki dunia papohapo huku wifi yake,  Jamhuri Makoi akifia Hospitali ya Rufaa ya KCMC, Moshi na mtoto wa marehemu, Brayan Makoi aliyekuwa amekaa siti ya nyuma akijeruhiwa vibaya. Hadi sasa amelazwa chumba cha uangalizi maalum (ICU) hospitalini hapo.
Marehemu Carista ambaye siku ya tukio alivaa shati maafuru kwa jina la ‘makenzi’ rangi ya bluu na nyeupe, aliumia kichwani na kifuani na alibanwa na bodi ya gari kiasi kwamba, ili kuutoa mwili wake ilibidi wasamaria wema kutumia shoka kukata mabati sanjari na kuondoa paa la gari hilo.
KAMANDA WA POLISI
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema dereva wa basi bado anashikiliwa na polisi kwa uchunguzi zaidi.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini