Daktari aliyetandikwa na wananchi baa avuliwa cheo



Wagonjwa wakimtia adabu Mganga Mkuu wa Kituo cha Afya cha Nyakabale mkoani Geita, Josephat Msafiri baada ya kuwatelekeza juzi. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Magreth Nakainga amemvua madaraka Mganga Mkuu wa Zahanati ya Nyakabale, Josephat Msafiri kwa kukiuka miiko ya kazi yake na kulewa wakati wa kazi.

Mkurugenzi huyo aliamua kuchukua uamuzi huo jana kutokana na tukio lililotokea Juzi hii la daktari huyo kufunga kituo cha afya na kuacha wagonjwa wakiwa wamezidiwa, kisha kwenda kunywa pombe jambo lililowalazima kumchapa viboko akiwa baa.
“Tumeshamchukulia hatua za kinidhamu ikiwa ni pamoja na kumvua madaraka yake ili iwe fundisho kwa watumishi wengine wa Serikali,” 
alisema Nakainga.

Alisema kitendo alichokifanya kimeidhalilisha taaluma ya afya na madaktari kwa ujumla.

Alisema tabia kama hizo hazitavumilika kwa mtumishi yeyote atakayekiuka maadili ya kazi.

Pia alisema amepeleka wahudumu wa afya wakiwamo wauguzi wawili na daktari mmoja katika zahanati hiyo na huduma zinaendelea vizuri.

Alipopigiwa simu jana ili azungumzie uamuzi huo, daktari huyo alianza kumlaumu mwandishi aliyeandika habari ya tukio hilo akisema kuwa amemharibia kazi.
“Sikutegemea kama wewe uko hivyo, sasa nimekujua kumbe uko hivyo, Mungu mkubwa, yaani mmepigiwa simu na watu na kuamua kuja kuniharibia,” alisema Dk Msafiri na kukata simu kisha akaandika ujumbe uliosema: “Sikukujua sasa nimekujua vizuri, Mungu mkubwa.” 

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini