Kigogo Mnyarwanda Chadema akamatwa, kisa si mtanzania

Gaudence Msuya, Mbogwe
MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilaya ya Mbogwe mkoani Geita, Omari Athanas, ametiwa mbaroni na maofisa uhamiaji wilayani hapa, akituhumiwa kwa uhamiaji haramu.
Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe, Aman Mwenegoha, alisema mwenyekiti huyo alikamatwa Desemba 22, mwaka huu na kuhojiwa na maofisa hao, ambapo alihojiwa kwa muda na kugundulika kwamba, si Mtanzania bali ni raia wa nchi jirani ya Rwanda.
Alisema taarifa ya kumbaini kuwa, si Mtanzania zilijitokeza wakati wa kampeni za Serikali za Mitaa, baada ya mwenyekiti huyo wa Chadema kwenda katika Kijiji cha Lugunga, ambapo inadaiwa kuna Wanyarwanda wengi na kuwahamasisha wafanye vurugu na kwamba, wasichague CCM kwa kuwa, Serikali haitaki kuwapa kibali cha uraia.
Kaimu mkuu huyo wa wilaya alisema baada ya mahojiano ya siku tatu, ndipo maofisa uhamiaji wa wilaya hiyo walipojiridhisha kuwa, si raia wa Tanzania.
Mwenegoha alisema Desemba 26, mwaka huu waliamua kumsafirisha nchini Rwanda, ambapo maofisa uhamiaji nchini humo walimtambua kuwa ni Mnyarwanda, na ana familia yenye mke na watoto wawili.
 
“Baada ya kumfikisha Rwanda, maofisa uhamiaji walimhoji ambapo walimtambua kuwa, ni raia wa nchi hiyo na wakati akija Tanzania walimpa kitambulisho, zaidi ya miaka 15 iliyopita na pia wakamgundua kuwa, ana familia yenye mke na watoto wawili,” alisema Mwenegoha.
Alifafanua kuwa, alifika nchini toka mwaka 2000 na kuishi katika Kitongoji cha Manzese Kata ya Busoka wilayani Kahama, na baadaye mwaka 2003 alihamia katika Kijiji cha Lugunga wilayani Mbogwe mkoani Geita, ambapo aliishi huko hadi alipokamatwa Jumatatu wiki hii.
Kuhusu wahamiaji waliopo katika wilaya hiyo, Mwenegoha alisema ni 14, ndiyo walioomba kuukana uraia wao na kupewa uraia wa Tanzania na kwamba, inadaiwa kuwa, ameacha deni la sh. milioni 1.5 ambalo anadaiwa na aliyekuwa Katibu Mwenezi wa Chadema wilayani humo, ambaye alihamia CCM, ambapo alikopa ili afanikishe kampeni za uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
Aidha, alisema katika tukio hilo imebainika kuwepo uzembe mkubwa uliofanywa na uhamiaji wilayani humo kwa kushindwa kumbaini mapema kiongozi huyo, ambapo alisema atakaa na kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya hiyo ili kujadili suala hilo.
Hata hivyo, Mwenegoha alisema kwa sasa wanajipanga kufanya oparesheni kubwa ya kuwasaka wahamiaji wote haramu ili sheria ichukue mkondo wake, ikiwemo kuwarudisha kwao watakaobainika.
Kwa upande wake, Ofisa Uhamiaji wilayani hapa, David Magwaza alisema wamebaini kuwa, mwenyekiti huyo aliingia nchini kijanja na kisha kujifunza lugha ya kiswahili fasaha.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chadema mkoani Geita, Alfonce Mawazo, alisema hizo ni siasa, huku akihoji kwanini hakukamatwa wakati wote huo alioishi nchini na badala yake, akamatwe sasa.
Alisema mwenyekiti huyo aliishi nchini kwa muda mrefu, ambapo ana mke na watoto wawili pia.

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini