Mauaji ya ‘Tajiri Mtoto’ yaendelea kuzua utata




Mtandao wa kikundi kinachozalisha pombe kali bandia kinachodaiwa kuwa na uhusiano na baadhi ya watumishi wasiowaaminifu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), unahusishwa na mipango ya kumuua mfanyabiashara Joseph Mahole maarufu ‘Tajiri Mtoto’. 
Mfanyabiashara huyo aliuawa kwa kupigwa risasi usiku wa kuamkia Desemba 30, mwaka jana nyumbani kwake eneo la Katanini, Wilaya ya Moshi Mjini. Mauaji hayo ambayo yameibua utata hasa baada ya wauaji hao kudaiwa kuondoka na bastola tu iliyokuwa ikimilikiwa na marehemu na hawakuchukua kitu kingine chochote. 
Habari kutoka kwa marafiki wa karibu na marehemu, zinadai huenda njama za kumuua zilifanywa na baadhi ya watumishi wa TRA na wafanyabiashara wanaozalisha pombe kali bandia. Kwani baada ya upekuzi uliofanyika nyumbani kwa Mahole, Polisi waligundua kuwapo kwa malighafi ya kutengenezea pombe kali pamoja na vifungashio vyake. Pia, walizikuta stika zenye nembo ya TRA zinazobandikwa kwenye chupa za pombe kuonyesha kuwa bidhaa inayouzwa imelipiwa kodi. Baada ya Mahole kuwagomea, watu hao walihofia kama angekamatwa angeweza kuwataja, 

hivyo wakaamua kumuua. Hata hivyo, bado utata unaendelea kugubika tukio hilo kwani inadaiwa kuwa marehemu hakuwahi kufanya biashara ya pombe, bali alikuwa akifanya biashara ya vifaa vya ujenzi na alikuwa akisafiri mara kwa mara kwenda China kununua bidhaa hizo. Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Ramadhan Mungi jana alisema wanaendelea kuchunguza mazingira ya kifo pamoja na vitu vilivyokamatwa baada ya upekuzi kufanyika nyumbani kwa marehemu zikiwamo stika hizo za TRA kama ni za mamlaka hiyo. 
“Ni kweli kulikutwa hizo stika na sisi kazi yetu ni kuchunguza ili kubaini zilifikaje nyumbani kwa marehemu,” alisema Mungi. Meneja wa TRA Mkoa wa Kilimanjaro, Abdul Mapembe alisema wao kama TRA hawajapewa taarifa kamili juu ya kupatikana kwa stika hizo nyumbani kwa Mahole. “Tunasikia taarifa hizo mitaani, lakini polisi bado hawajatueleza chochote,” alidai Mapembe. Alisema watawasiliana na Polisi kama inawezekana, watakwenda kuzitambua kama ni mali ya TRA ama la.


ASANTE KWA KUTEMBELEA MTANDAO WETU!!

Popular posts from this blog

Upepo wakwamisha Uokoaji Meli iliyozama

Walimu wadaiwa kuacha vipindi kukimbilia kufanya kazi migodini